USEMI WA WASHIRIKI WA TUZO YA FASIHI ZA KIAFRIKA YA MABATI-CORNELL KUHUSU KUSHIKILIWA KWA RANGIMOTO.

Sisi washiriki wa tuzo tajwa hapo juu, tumepokea kwa mshituko na masikitiko makubwa habari za kushikiliwa mshiriki mwenzetu, Bwana Dotto Rangimoto, na Mamlaka nchini Tanzania katika namna ambayo tunaamini inavunja haki zake za kisheria na pia za kibinaadamu.
Tokea tarehe 25.09.2020, Bwana Dotto Rangimoto yuko mikononi kwa vyombo vya dola, ambako, kwa mujibu wa taarifa tunazopokea haruhusiwi kuonana na ndugu wala wanasheria wanaomuwakilisha.
Kwa umoja wetu, sisi wanafasihi ambao tuliwahi kuwa katika orodha za washiriki wa Tuzo za Kiswahili za Fasihi ya Afrika za Mabati-Cornell, tunaziomba mamlaka husika aidha kumuachilia huru Dotto Rangimoto ama kumpeleka mahakamani kwa mujibu wa sheria za nchi, ambazo zinakataza mtu yeyote kuwa chini ya mikono ya vyombo vya dola kwa zaidi ya saa 24 bila kushitakiwa.
Tunaomba kama lipo ambalo anatuhumiwa kwalo, basi mchakato wa kesi yake uendeshwe kwa haki na kwa dhana kwamba hana makosa kwa mujibu wa sheria hadi pale mahakama itakapoamuru vinginevyo.
Imetiwa sahihi na:
1. Mohammed Khelef Ghassani
2. Anna Samuel
3. Enock Maregesi
4. Ali Hilal
5. Nassor Hilal
6. Ahmed Hussein Ahmed
7. Mbarouk Ally
8. Bashiru Abdallah
9. Zainab Baharoon
10. Jacob Ngumbau Julius
11. Mohammed Khamis Songoro
12. Rashid Othman
13. Yasin Sheki